" MTAALA WA MAMA WA UPENDO NA PROGRAM YA ALPHA KUIMARISHA MALEZI YA KIROHO KWA VIJANA WAZINDULIWA

MTAALA WA MAMA WA UPENDO NA PROGRAM YA ALPHA KUIMARISHA MALEZI YA KIROHO KWA VIJANA WAZINDULIWA


Vituo vya maendeleo ya mtoto na kijana katika Klasta ya Shinyanga vimezindua mtaala wa Mama wa Upendo pamoja na program ya Alpha, hatua inayolenga kuimarisha malezi ya kiroho kwa watoto na vijana na kuwasaidia kufuata misingi sahihi ya maisha.

Akizungumza wakati wa uzinduzi huo, Mwezeshaji wa Klasta ya Shinyanga na Kahama, Bwana Remi Dumbi, alisema miongozo hiyo imelenga kuwawezesha wamama wa upendo kutekeleza majukumu yao kwa ufanisi zaidi katika kuwalea na kuwaombea watoto pamoja na vijana.

Alisema kuna umuhimu mkubwa wa kuwaombea vijana katika kila hatua ya maisha yao, akibainisha kuwa hata wanapofikisha umri wa miaka 20 na kuendelea bado wanahitaji maombi na uongozi wa kiroho.
“Lengo letu la kwanza ni kuhakikisha vijana wanamjua Yesu na kufuata njia sahihi. Wamama wa upendo wamekuwa mstari wa mbele katika maombi na tunawashukuru kwa hilo,” alisema.

Aliongeza kuwa mtaala wa Mama wa Upendo unahusisha masuala ya utume wa mama, majukumu yao, namna ya kufundisha, vipindi pamoja na mbinu za kushirikiana na watendakazi katika kuwalea vijana na kubaini maono yao.

Kwa upande wa program ya Alpha, Dumbi alisema Klasta hiyo imeingia makubaliano na shirika la Alpha tangu mwezi Machi kwa lengo la kuwafikia vijana ambao mara nyingi hawapendi kuhudhuria ibada makanisani.
Alisema kupitia program hiyo, vijana hao wanatafutwa na kuandaliwa mazingira rafiki ya kuwavuta na kuwasaidia kumjua Yesu.

Aidha, Askofu wa Kanisa la Anglikana Tanzania, Steven Chinyongolo, aliwataka vijana kutumia fursa hiyo kujijenga kiroho na kuwa na hofu ya Mungu katika maisha yao, huku akiwahimiza wamama wa upendo kuendelea kuwa nguzo muhimu katika malezi ya kizazi kijacho.

Naye Mchungaji Odras aliwataka washiriki wa tukio hilo kumtumaini Mungu na kuomba uongozi wake katika utekelezaji wa mtaala huo, akisisitiza kuwa malezi ya kiroho ni msingi muhimu wa maisha ya mwanadamu na yanapaswa kupewa kipaumbele.

Wakati huo huo, Wamama wa Upendo wa huduma ya Esta Encounter katika Klasta ya Shinyanga wameeleza mafanikio, changamoto na matarajio yao katika kuimarisha huduma ya mtoto na kijana, wakisisitiza umuhimu wa ushiriki wa wanawake wa Kikristo katika malezi na ulinzi wa watoto.

Huduma hiyo ilianzishwa mwaka 2008 na Mchungaji Emmanuel Mbennal, aliyekuwa Mkurugenzi wa Nchi wa Compassion International Tanzania, kwa lengo la kuwawezesha wanawake kushiriki kikamilifu katika huduma ya watoto na vijana kupitia maombi, malezi na ushauri wa kijamii.

Wamama hao wamesema wamefanikiwa kuunda uongozi, kuendesha mikutano ya maombi ya mara kwa mara na kushiriki katika shughuli za kuwalea na kuwaombea watoto na vijana, huku wakiimarisha mshikamano kwa kusaidiana wakati wa changamoto.

Hata hivyo, wamebainisha changamoto zinazowakabili kuwa ni pamoja na mwitikio mdogo wa baadhi ya wanachama, ukosefu wa fedha za usafiri, ushirikiano hafifu kutoka baadhi ya watendakazi pamoja na uhaba wa vitabu vya muongozo wa huduma.

Pamoja na changamoto hizo, wamama hao wameeleza kuwa wanaendelea kushikamana na kuamini kuwa kupitia umoja na ushirikiano, huduma hiyo itaendelea kukua na kuleta matokeo chanya kwa watoto na vijana katika jamii.






SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

 
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254


Post a Comment

Previous Post Next Post