" MTOTO WA MIAKA 10 AOKOLEWA DHIDI YA UKATILI BAADA YA KUKIMBILIA KWA KATIBU SMAUJATA MSALALA

MTOTO WA MIAKA 10 AOKOLEWA DHIDI YA UKATILI BAADA YA KUKIMBILIA KWA KATIBU SMAUJATA MSALALA

Katibu wa Jumuiya ya Shujaa wa Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Halmashauri ya Msalala wilayani Kahama, mkoani Shinyanga, Bi. Nives Nyoni, ameongoza juhudi za uokoaji wa mtoto wa kike mwenye umri wa miaka 10 aliyedaiwa kukumbwa na vitendo vya ukatili kutoka kwa mama yake mzazi.

Tukio hilo lilitokea Aprili 23, 2026 majira ya saa mbili usiku katika kijiji cha Isaka Station, ambapo mtoto huyo alikimbilia nyumbani kwa Bi. Nyoni kuomba msaada, akieleza kuwa amekuwa akipigwa mara kwa mara, kunyimwa haki ya masomo pamoja na kufanyiwa vitendo vya mateso.

Baada ya kupokea taarifa hiyo, Bi. Nyoni alimpatia hifadhi ya muda mtoto huyo nyumbani kwake na kuwashirikisha viongozi wengine wa SMAUJATA akiwemo Mwenyekiti wa SMAUJATA Mkoa wa Shinyanga Bi. Nabila Kisendi ambapo Asubuhi iliyofuata, kwa kushirikiana na mtoto huyo, walimpeleka katika kituo cha polisi kwa ajili ya hatua zaidi dhidi ya mzazi anayetuhumiwa.

Katika kufanikisha zoezi hilo, SMAUJATA ilishirikiana na maafisa ustawi wa jamii wa Halmashauri ya Msalala akiwemo Afisa Richard Ng’ondya, Ignace Lufulila pamoja na Bi. Magori, watendaji wa eneo husika na mkuu wa kituo cha polisi, ambapo kwa pamoja walitafuta suluhisho la kudumu kwa mtoto huyo.

Baada ya tathmini, ilibainika kuwa mama mzazi wa mtoto huyo ana changamoto ya afya ya akili, hali iliyochangia kuchukuliwa kwa uamuzi wa kumkabidhi mtoto kwa baba yake mzazi anayeishi Misungwi, mkoani Mwanza.

Mwenyekiti wa SMAUJATA, Nabila Kisendi, pamoja na Mwenyekiti wa Kata, Bi. Sophia Emanuel, walisisitiza umuhimu wa mzazi huyo wa kiume kuhakikisha anampatia mtoto malezi bora, huku wakiahidi kuwa taasisi hiyo itaendelea kufuatilia ustawi wa mtoto huyo hata baada ya kuhamishiwa kwa baba yake.

Imeelezwa kuwa mtoto huyo, alionyesha hitaji kubwa la kuishi na baba yake tofauti na ilivyo kwa watoto wengi wanaopendelea malezi ya mama, hali iliyotafsiriwa kuwa ni matokeo ya mazingira magumu aliyokuwa akipitia.

Kwa mujibu wa taarifa, mtoto huyo alikumbwa na ukatili uliodaiwa kujumuisha kupigwa, kubamizwa ukutani na kufanyiwa vitendo vingine vya mateso, hali iliyomlazimu kutafuta msaada.

SMAUJATA imewapongeza maafisa na wadau wote walioshiriki katika zoezi hilo kwa ushirikiano wao, huku wakisisitiza kuendelea kupinga ukatili dhidi ya watoto na kuhakikisha haki zao zinalindwa.

 SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment

Previous Post Next Post