" MWENYEKITI CHADEMA KANDA YA SERENGETI AAGIZA NIDHAMU, UWAJIBIKAJI; VIONGOZI WASISITIZA TUNDU LISSU AACHIWE

MWENYEKITI CHADEMA KANDA YA SERENGETI AAGIZA NIDHAMU, UWAJIBIKAJI; VIONGOZI WASISITIZA TUNDU LISSU AACHIWE

Na Mapuli Kitina Misalaba

Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Serengeti, Lucas Ngoto, ametoa maelekezo mbalimbali kwa viongozi na wanachama wa chama hicho akisisitiza nidhamu, uwajibikaji na kujitegemea kiuchumi, huku akionya kuwa uongozi usiofanya kazi hautavumiliwa.

Ngoto ametoa maelekezo hayo wakati wa hafla ya uzinduzi wa shughuli za chama na ukarabati wa ofisi ya kanda iliyofanyika mkoani Shinyanga, Aprili 26, 2026 ambapo amewataka viongozi wote kuanzia ngazi ya mkoa, wilaya, kata hadi matawi kutekeleza majukumu yao kikamilifu.

Amesema ni lazima kila kiongozi awajibike katika nafasi yake na kuhakikisha chama kinaendelea kuwa imara, akisisitiza kuwa wale watakaoshindwa kuwajibika wataondolewa ili kupisha wengine wenye uwezo.

“Mtu yoyote ambaye hatakuwa anawajibika hatutamvumilia, tutawaondoa ili kutoa nafasi kwa wengine wanaoweza kusimamia majukumu yao ipasavyo,” amesema Ngoto.

Aidha, amewataka viongozi wa ngazi ya mkoa kusimamia viongozi wa wilaya, huku wale wa wilaya wakisimamia kata na matawi ili kuhakikisha uwajibikaji unazingatiwa katika kila ngazi ya uongozi.

Katika kusisitiza mshikamano wa chama, Ngoto ameeleza kuwa nidhamu ni msingi muhimu wa mafanikio, akibainisha kuwa chama hakiwezi kusonga mbele bila kuwepo kwa heshima na ushirikiano miongoni mwa wanachama wake.

“Nasisitiza suala la nidhamu, kila mmoja amheshimu mwenzake, chama kisicho na nidhamu hakiwezi kufikia malengo yake,” amesema Ngoto

Pia ametoa wito kwa wanachama, hususan vijana na wanawake, kujishughulisha na shughuli za kiuchumi ili kujiepusha na utegemezi unaoweza kuwafanya kushawishika kirahisi kisiasa.

Amesisitiza kuwa katika uongozi wake hataki kuona wanachama wasiokuwa na shughuli za kuwaingizia kipato, akiwahimiza kufanya kazi ndogo ndogo zitakazowawezesha kujitegemea.

“Napenda wanachama wanaofanyakazi, kila mmoja ahakikishe anatafuta kipato chake, hali ya utegemezi inaweza kudhoofisha misimamo ya chama,” amesema.

Ngoto pia amewataka wanachama kujiepusha na tamaa za madaraka, akieleza kuwa baadhi ya waliokuwa viongozi walihama chama wakaahidiwa nafasi mbalimbali ambazo hadi sasa hawajazipata.

Katika hatua nyingine, ametangaza kuwa chama kina mpango wa kufanya chaguzi za kujaza nafasi zilizo wazi ndani ya chama, ambapo amewahimiza wanachama kujitokeza kwa wingi kugombea nafasi hizo pindi tarehe rasmi itakapotangazwa.

“Tunazo nafasi wazi, chama kina watu bora kabisa wa kujaza nafasi hizo, hivyo jitokezeni kugombea ili kuendeleza mapambano ya chama,” amesema Ngoto.

Awali kabla ya hotuba ya mwenyekiti, Katibu wa CHADEMA Kanda ya Serengeti, Jackson Mnyawami, alitoa taarifa fupi akieleza sababu za kuanza kwa mpango wa ukarabati wa ofisi ya kanda, akibainisha kuwa hatua hiyo inalenga kuboresha mazingira ya kazi na kuongeza ufanisi wa utendaji wa chama.

Amesema ukarabati na upanuzi wa ofisi ya CHADEMA Kanda ya Serengeti, ni sehemu ya juhudi za kuimarisha miundombinu na shughuli za chama katika ukanda huo.

Hafla hiyo imehudhuriwa na viongozi mbalimbali kutoka mikoa ya Shinyanga, Mara na Simiyu, ambapo baadhi yao walipata nafasi ya kuzungumza na kusisitiza umuhimu wa mshikamano ndani ya chama.

Katika hotuba zao, viongozi hao pia walisisitiza serikali kumwachia Mwenyekiti wa CHADEMA taifa, Tundu Lissu, ili aweze kuendelea na majukumu yake ya uongozi ndani ya chama.Katibu wa CHADEMA Kanda ya Serengeti, Jackson Mnyawama, akitoa taarifa fupi kuhusu mpango wa ukarabati wa ofisi ya kanda.Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Serengeti, Lucas Ngoto, akizungumza na viongozi na wanachama wakati wa uzinduzi wa ukarabati wa ofisi ya kanda uliofanyika mkoani Shinyanga.Mwenyekiti wa CHADEMA Kanda ya Serengeti, Lucas Ngoto, akisalimiana na viongozi mbalimbali wa chama mara baada ya kuwasili kwenye hafla ya uzinduzi mkoani Shinyanga.


SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

 

Post a Comment

Previous Post Next Post