Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya
Mpanda imefanya kikao chake Juni 24, 2026 kwa lengo la kujadili masuala
mbalimbali yanayohusu maendeleo na uhai wa jumuiya hiyo pamoja na kufanya
maandalizi ya Baraza la Wazazi la Wilaya litakalofanyika Juni 25, 2026.
Kikao hicho kilijadili kwa kina suala la kuimarisha
uhai wa Jumuiya ya Wazazi, ambapo wajumbe walisisitiza umuhimu wa viongozi na
wanachama katika ngazi zote kuendelea kulipia ada za uanachama ili kuhakikisha
jumuiya inaendelea kuwa hai na kutekeleza majukumu yake kwa ufanisi.
Aidha, wajumbe walijadili mikakati ya kuongeza idadi
ya wanachama kupitia kampeni ya usajili katika matawi na kata mbalimbali za
Wilaya ya Mpanda. Kikao hicho kilikubaliana kuwa viongozi wa jumuiya kwa
kushirikiana na maafisa wa TEHAMA watembelee maeneo mbalimbali kutoa elimu
kuhusu namna ya kujiunga na jumuiya na kulipia ada kwa njia za kidijitali,
ikiwemo simu, mawakala na benki.
Katika kikao hicho, wajumbe pia walijadili hatma ya
Shule ya Sekondari na Ufundi Milala iliyopo Kijiji cha Milala, Kata ya
Misunkumilo, ambayo imekuwa haifanyi kazi kwa kipindi cha takribani miaka
mitano. Wajumbe walieleza kuwa shule hiyo ni mali ya Jumuiya ya Wazazi Wilaya
ya Mpanda na kuna haja ya kuendelezwa ili iweze kutoa mafunzo mbalimbali ya
elimu na ufundi kwa vijana.
Kamati hiyo ilibaini kuwa changamoto kubwa inayokabili
shule hiyo ni ukosefu wa hati miliki ya eneo pamoja na gharama za upimaji wa
eneo hilo zinazokadiriwa kufikia shilingi milioni 2.3. Wajumbe walisisitiza
kuwa hakuna mgogoro wowote kati ya shule hiyo na taasisi nyingine kama ambavyo
baadhi ya wananchi wamekuwa wakidai, na kwamba juhudi zinaendelea kufanyika ili
kupata hati miliki na kuendeleza shule hiyo.
Kutokana na hali hiyo, Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya
Mpanda imewaomba wadau mbalimbali wa maendeleo kujitokeza kusaidia juhudi za
kuendeleza shule hiyo kwa manufaa ya jamii na kizazi kijacho.
Kikao hicho pia kilijadili miradi mbalimbali ya
kiuchumi inayolenga kuongeza uwezo wa kifedha wa jumuiya. Wajumbe walihimizwa
kubuni na kuanzisha miradi katika ngazi za matawi na kata ili kuongeza vyanzo
vya mapato na kuifanya jumuiya kujitegemea zaidi.
Kwa upande mwingine, kamati ilipokea taarifa ya
tathmini ya Maadhimisho ya Wiki ya Wazazi yaliyofanyika Mei 7, 2026 katika
Hospitali ya Halmashauri ya Nsimbo, Kata ya Mtapenda. Wajumbe walieleza
kuridhishwa na mafanikio ya maadhimisho hayo yaliyohusisha utoaji wa misaada
kwa wagonjwa pamoja na upandaji wa miti ya matunda na kivuli.
Maadhimisho hayo yaliongozwa na Mwenyekiti wa Jumuiya
ya Wazazi Mkoa wa Katavi, Ndugu Evarist Simon Mnyele, na kuhudhuriwa na
viongozi mbalimbali wa Serikali na Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Katika maandalizi ya Baraza la Wazazi Wilaya ya Mpanda
litakalofanyika Juni 25, 2026, kamati ilisisitiza umuhimu wa kutekeleza
majukumu ya jumuiya kwa mujibu wa katiba, kanuni na maelekezo ya chama. Pia
ilipendekeza kuendelea na ziara za viongozi katika matawi na kata kwa lengo la
kutoa elimu kuhusu malezi, mazingira na kuimarisha uhai wa jumuiya.
Wajumbe walijadili pia maandalizi ya ushiriki wa
Wilaya ya Mpanda katika Maadhimisho ya Wiki ya Wazazi Kitaifa yatakayofanyika
Mkoani Mwanza kuanzia Juni 30 hadi Julai 4, 2026. Kamati ilieleza umuhimu wa
wanachama kushiriki maadhimisho hayo ili kuimarisha mshikamano na kubadilishana
uzoefu na wanachama kutoka maeneo mbalimbali nchini.
Akizungumza katika kikao hicho, Katibu wa Jumuiya ya
Wazazi Wilaya ya Mpanda, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka, aliwataka viongozi na
wanachama kuendelea kudumisha umoja na mshikamano huku wakihamasisha wanachama
wengi zaidi kushiriki katika maadhimisho ya kitaifa ya Wiki ya Wazazi
yatakayofanyika Mwanza.
Amesema umoja na mshikamano ni msingi muhimu wa
mafanikio ya jumuiya na Chama Cha Mapinduzi, hivyo kila mwanachama ana wajibu
wa kushiriki kikamilifu katika shughuli mbalimbali zinazolenga kuimarisha
maendeleo ya jumuiya na jamii kwa ujumla.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya
Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda, Ndugu Pius M. Buzumalle, akifungua kikao cha
Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda leo Juni 24,
2026, saa 4:30 asubuhi, kilicholenga kufanya maandalizi ya Baraza la Wazazi Wilaya
ya Mpanda litakalofanyika Juni 25, 2026. Katika ufunguzi wake, aliwataka
wajumbe kuwa watulivu, kufuatilia agenda za kikao na kutoa michango yenye
kujenga kwa maendeleo ya Jumuiya.

Katibu wa Jumuiya ya Wazazi
CCM Wilaya ya Mpanda, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka, akiwakaribisha na
kuwashukuru wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi Wilaya ya
Mpanda katika kikao cha maandalizi ya Baraza la Wazazi Wilaya ya Mpanda
kinachotarajiwa kufanyika Juni 25, 2026. Aidha, aliwasisitiza wajumbe kuwa na
usikivu mzuri na kushiriki kikamilifu kwa kutoa mawazo na michango yenye
kujenga katika kikao hicho kilichofanyika Juni 24, 2026.

Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda, Ndugu Pius M. Buzumalle, leo Juni 24, 2026 akiongoza kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda kilicholenga kufanya maandalizi ya Baraza la Wazazi Wilaya ya Mpanda, ambalo linatarajiwa kufanyika Juni 25, 2026.
Kikao hicho kimejadili masuala mbalimbali ya utekelezaji wa majukumu ya Jumuiya pamoja na kuimarisha uhai na maendeleo ya Jumuiya ya Wazazi ndani ya Wilaya ya Mpanda.
Wajumbe wa Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda wakifuatilia kwa umakini kikao cha maandalizi ya Baraza la Wazazi Wilaya ya Mpanda, kilichofanyika Juni 24, 2026, kuelekea Baraza la Wazazi la Wilaya linalotarajiwa kufanyika Juni 25, 2026.
Katibu wa Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda, Ndugu Jimotoli Jilala Maduka, akishiriki kikamilifu kikao cha Kamati ya Utekelezaji ya Jumuiya ya Wazazi CCM Wilaya ya Mpanda kilichofanyika Juni 24, 2026, kwa ajili ya maandalizi ya Baraza la Wazazi Wilaya ya Mpanda linalotarajiwa kufanyika Juni 25, 2026.SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254



Post a Comment