" RUWASA SHINYANGA YAKABIDHI MTAMBO WA KISASA WA KUCHIMBA VISIMA VYA MAJI, RC MNDEME ATAKA WANANCHI KUTUNZA MIUNDOMBINU

RUWASA SHINYANGA YAKABIDHI MTAMBO WA KISASA WA KUCHIMBA VISIMA VYA MAJI, RC MNDEME ATAKA WANANCHI KUTUNZA MIUNDOMBINU

Na Mapuli Misalaba, Shinyanga

Serikali ya Mkoa wa Shinyanga imepokea mtambo wa kisasa utakaotumika kuchimba visima vya maji, kwa fedha za mradi wa  Uviko 19 ambao utawanufaisha wananchi  katika Wilaya ya Kishapu pamoja na Halmashauri ya Ushetu.

Katika taarifa yake wakati akikabidhi mtambo huo, Meneja wa wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini RUWASA Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Julieth Payovela amesema Mkoa wa Shinyanga ni moja ya Mikoa inayokabiliwa na ukame kutokana na sababu mbalimbali.

Mhandisi Payovela ameeleza kuwa Mkoa wa Shinyanga pamoja na kunufaika na mradi wa maji ya ziwa Victoria lakini bado yapo baadhi ya maeneo yenye changamoto ya maji ambapo ili kutatua changamoto hiyo serikali  imenunua mitambo 25 itakayotumika kuchimba mabwawa ya maji.

“Mkoa wa Shinyanga ni moja ya mikoa kame (semi – arid Region ), kutokana na hali hiyo upatikanaji wa vyanzo vya maji chini ya ardhi imekuwa changamoto hata hivyo Mkoa wa Shinyanga ni mnufaika wa kwanza wa mradi wa maji ya ziwa Victoria ambao kwa sasa unahudumia mikoa ya Mwanza (Kwimba na Misungwi), Shinyanga, Tabora (Igunga, Tabora na Nzega) na mji wa Shelui Mkoa wa Singida”. amesema Mhandisi Julieth Payovela

“Ujenzi wa miradi ya maji kupitia bomba kuu la KASHWASA umeendelea hadi sasa jumla ya vijiji 89 vinapata maji na vijiji 50 ujenzi wa miundombinu ya kusambaza maji kupitia bomba hilo upo katika hatua mbalimbali za utekelezaji”.

“Uunganishaji wa maji ya KASHWASA umeendelea kufanyika kwa vijiji vilivyondani ya umbali wa km 12 kutoka bomba kuu la KASHWASA katika vijiji vilivyombali zaidi na mtambo wa KASHWASA tumeendelea kufanya utafiti wa maji chini ya ardhi na uchimbaji wa visima virefu”. amesema Mhandisi Julieth Payovela

Meneja huyo wa RUWASA Mkoa wa Shinyanga amesema Mhandisi Julieth Payovela ametaja Wilaya zitakazonufaika na  uchimbaji visima katika Mkoa wa Shinyanga kuwa ni kishapu na kahama katika halmashauri ya Ushetu.

“Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan imenunua mitambo 25 na seti 5 ya kuchimba mabwawa  ya maji iliyonunuliwa na Rais Dkt. Samia kupitia wizara ya maji kwa fedha za Uviko – 19, mtambo huu ambao tumeukabidhi leo ni moja ya mitambo iliyonunuliwa kwa ajili ya uchimbaji wa visima mtambo huu unauwezo wa kuchimba kisima hadi mita 300”.amesema Mhandisi Julieth Payovela

“Aidha kupitia fedha za Uviko 19 Mkoa wa Shinyanga ulitekeleza miradi ya maji, mradi mmoja kila jimbo isipokuwa jimbo la Solwa imejengwa miradi miwili jumla ya fedha kiasi cha Tsh. 3061,459,641.73 zimetumika kutekeleza miradi saba (7) miradi yote imekamilika na wananchi 26,902 wanapata huduma”.

“Mtambo huu tunaoukabidhi kwa kuanza na uchimbaji utaanza katika vijiji vinne (4) kijiji cha Itilima na Mwashinongela vya Wilaya ya Kishapu na Ubagwe na Kinamapula vya Halmashauri ya Ushetu”.amesema Mhandisi Julieth Payovela

Kwa upande wake Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Christina Mndeme amemshukuru Rais wa jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuleta mtambo huo wa maji ambao utasaidia kutatua kero kwa wananchi.

RC Mndeme amewaomba RUWASA kusimamia na kutekeleza  mradi huo kwa kuhakikisha unaleta matokeo chanya kama ulivyokusudiwa huku akiwaomba wananchi wa Mkoa wa Shinyanga hasa watakaofikiwa kutunza miundombinu ya mtambo huo.

“Niwaombe RUWASA mtambo huu ukatumike kwa malengo yaliyokusudiwa lakini kabla ya kuchimba kisima tuhakikishe tunafanya uchunguzi wa kina ili kujua tunapochimba kweli maji yapo kuliko tutumie gharama kupeleka mtambo kwenda kuchimba maji kumbe maji hamna”.

“Vile vile niwaomba wananchi kwa pamoja tutunze miundombinu ambayo itawekwa ya maji katika maeneo yetu na vile vile tutunze mazingira ili tunufaike sisi na vizazi vijazo”.amesema RC Mndeme

Meneja wa wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini RUWASA Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Julieth Payovela  akisoma taarifa yake wakati wa hafla ya kukabidhi mtambo huo.

 Meneja wa wakala wa maji na usafi wa mazingira vijijini RUWASA Mkoa wa Shinyanga Mhandisi Julieth Payovela  akisoma taarifa yake wakati wa hafla ya kukabidhi mtambo huo.

Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Christina Mndeme akizungumza katika hafla hiyo

Wa kwanza upande wa kushoto ni Kaimu Meneja wa KASHWASA, John Zengo akifuatiwa na Meneja wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Vijijini (RUWASA) Mkoa wa Shinyanga, Mhandisi Julieth Payovela, Aliyevaa suti nyeusi wa pili kutoka upande wa kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Christina Mndeme akikata utepe kwenye hafla hiyo na wa kwanza upande wa kulia ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira Shinyanga (SHUWASA) Mhandisi Yusuph Katopola.








Post a Comment

Previous Post Next Post