Na Mapuli Kitina Misalaba
Timu ya Salawe FC imeibuka na ushindi wa goli moja
dhidi ya Mwasenge FC katika hatua ya nusu fainali ya Krismas Cup 2024,
mashindano yanayodhaminiwa na Makamba Mussa Lameck.
Kwa mujibu wa Bwana Placid Thomas, aliyetoa taarifa
kwa niaba ya msimamizi wa ligi hiyo, Salawe FC sasa watakutana na Beya FC
katika mchezo wa fainali utakaofanyika Jumanne, Desemba 17, 2024.
Aidha, Placid amesema kuwa Kano FC na Mwasenge FC
watashuka dimbani siku ya Jumatatu, Desemba 16, 2024, kushindania nafasi ya
tatu.
"Nawasisitiza
wananchi na timu zote kwa ujumla wanapokuja uwanjani wasije na matokeo kwa
sababu mpira ni mchezo wa wazi, yoyote anastahili kushinda," amesema
Placid.
Pia ameongeza kuwa kamati ya ligi inasimamia haki bila
upendeleo na kwamba rushwa haitavumiliwa. "Tunatarajia fainali na ligi hii
kwa ujumla imalizike salama," amesema Placid.
Viongozi wa timu mbalimbali pamoja na wachezaji wameendelea
kumpongeza Bwana Makamba Mussa Lameck kwa kuandaa mashindano haya, wakisema
kuwa ni fursa adhimu kwa maendeleo ya michezo mkoani Shinyanga ambapo wameomba
pia ligi hiyo iwe endelevu kila mwaka.
Fainali za Krismas Cup zinatarajiwa kuwa ya kipekee,
ambapo zawadi mbalimbali zitatolewa kwa washindi wa nafasi ya kwanza hadi ya
tatu.
Mashindano haya yanafadhiliwa na Makamba Mussa Lameck kupitia kampuni yake ya MCL, inayojishughulisha na biashara ya nafaka, kwa lengo la kuchochea maendeleo ya michezo katika jamii.

Post a Comment