" SHULE YA MSINGI KOLANDOTO YAMSHUKURU MOSES KWA KUCHANGIA SARUJI KWA AJILI YA UJENZI WA VYOO VYA WALIMU

SHULE YA MSINGI KOLANDOTO YAMSHUKURU MOSES KWA KUCHANGIA SARUJI KWA AJILI YA UJENZI WA VYOO VYA WALIMU

Na Mapuli Kitina Misalaba

 Mwalimu Mondesta Kilasa, akizungumza kwa niaba ya mkuu wa Shule ya Awali na Msingi Kolandoto katika Manispaa ya Shinyanga, amemshukuru na kumpongeza kijana Moses Mshagatile kwa moyo wake wa kizalendo baada ya kukabidhi mifuko ya saruji kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa vyoo vya walimu shuleni hapo.

Akizungumza wakati wa tukio hilo, Mwalimu Kilasa amesema msaada huo umetolewa katika wakati muafaka, kwani kwa muda mrefu shule hiyo imekuwa ikikabiliwa na changamoto ya ukosefu wa vyoo vya walimu hali iliyokuwa ikisababisha usumbufu mkubwa kwa walimu.

Kwa upande wake, Moses Mshagatile ambaye ni mzaliwa wa kata ya Kolandoto na pia ni mmoja wa wanafunzi waliopitia shule hiyo, amesema ameamua kujitokeza kusaidia baada ya kusikia kupitia vikao vya wazazi kuwa shule hiyo haina vyoo vya walimu, jambo lililomsukuma kuchangia ili kuweka mazingira mazuri ya kazi kwa walimu wanaolea kizazi kijacho.

Naye mzazi wa mwanafunzi katika shule hiyo, Sostenes John, amepongeza hatua ya Moses Mshagatile akisema ni mfano bora wa kuigwa na vijana wengine, hasa wale waliopitia shule hiyo na wana uwezo wa kusaidia kwa njia yoyote.

Ujenzi wa vyoo hivyo vya kisasa umeanza hivi karibuni baada ya uongozi wa shule kukutana na wazazi na wadau wa elimu kujadili namna ya kushughulikia changamoto hiyo ya muda mrefu.

Shule ya Awali na Msingi Kolandoto inaendelea kuwakaribisha wadau wengine wa maendeleo kuungana katika juhudi za kuboresha miundombinu ya shule hiyo.

Moses Mshagatile baada ya kuwasili katika Shule ya Awali na Msingi Kolandoto uliyopo  Manispaa ya Shinyanga, kwa lengo la kukabidhi msaada wa mifuko ya Saruji.

Moses Mshagatile akisaini kitabu cha wageni katika Shule ya Awali na Msingi Kolandoto uliyopo  Manispaa ya Shinyanga.


 

Post a Comment

Previous Post Next Post