" SAJENTI NDIMILA: KONDAKTA AKIZIDISHA ABIRIA, PAZENI SAUTI ZENU

SAJENTI NDIMILA: KONDAKTA AKIZIDISHA ABIRIA, PAZENI SAUTI ZENU

Abiria wa masafa marefu wamepewa elimu ya kutokukaa kimya pindi wanapoona vitendo vya kuzidisha abiria vikifanywa na makondakta kwenye magari ya usafiri wakati wa safari.

Akitoa elimu hiyo, Askari Polisi wa Kikosi cha Usalama Barabarani Mkoa wa Shinyanga, Sajenti David Ndimila, amewataka abiria kuwa mstari wa mbele katika kukemea na kuripoti vitendo hivyo ambavyo vimekuwa vikitokea mara kwa mara kwenye safari za masafa marefu.

“Abiria msikae kimya mnapoona makondakta wanazidisha abiria. Pazeni sauti zenu, mkemee vitendo hivyo kwa kuwa mkiendelea kunyamaza, mnashiriki moja kwa moja kuvunja sheria na kuhatarisha maisha yenu,” amesema Sajenti Ndimila.

Aidha, Sajenti Ndimila amesisitiza kuwa ushirikiano wa pamoja kati ya wananchi na vyombo vya usalama ndio njia pekee ya kudhibiti uvunjifu wa sheria za usalama barabarani, badala ya kuwaachia askari pekee jukumu hilo.

“Polisi peke yao hawawezi kufanikisha jambo hili bila ushirikiano wenu. Ni wajibu wenu kuhakikisha mnakuwa sehemu ya mapambano dhidi ya vitendo vya uvunjifu wa sheria barabarani,” ameongeza.

Elimu hiyo inalenga kupunguza ajali na madhara yanayotokana na tabia ya kuzidisha abiria, ambayo imekuwa chanzo cha migongano na ajali katika usafiri wa masafa marefu.

 

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

 

Post a Comment

Previous Post Next Post