Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Janeth Magomi.Na Mapuli Kitina Misalaba
Mwanamke mmoja mkazi wa Kijiji cha Songambele, Kata ya
Salawe, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, amefariki dunia katika mazingira ya
kutatanisha baada ya kukutwa na majeraha sehemu mbalimbali za mwili wake.
Taarifa za tukio hilo zimetolewa na Mwenyekiti wa
Kijiji cha Songambele, Razaro Enock, ambaye amesema tukio hilo limetokea katika
Kitongoji cha Machongo ambapo marehemu alikutwa akiwa amefariki huku chanzo cha
kifo hicho kikibaki kuwa kitendawili katika hatua za awali.
“Yule mama alifariki katika mazingira ya
kutatanisha, mwili wake ulikuwa na majeraha. Inasemekana alikuwa na mgogoro na
mume wake, ambaye hakuwepo nyumbani. Aidha, alidaiwa kuishi na mwanaume
mwingine aliyemtambulisha kama kaka yake, lakini baadaye ilibainika kuwa si
ndugu yake bali alikuwa na uhusiano wa kimapenzi naye,”
amesema Enock.
Ameongeza kuwa, baada ya muda mfupi wa kuishi pamoja,
wawili hao walitofautiana na mwanaume huyo kuondoka na mali zake, na muda mfupi
baadaye ndipo tukio hilo la kifo lilipotokea.
Kwa mujibu wa mwenyekiti huyo, watoto wa marehemu
walidai kuwa siku ya tukio mwanaume huyo alifika usiku na kuwahamasisha watoto
kulala mapema, jambo linalozua hisia kuwa huenda akawa na uhusika katika tukio
hilo.
Akizungumza na Misalaba Media, Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa
wa Shinyanga, Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Janeth Magomi,
amesema tukio hilo limethibitishwa kutokea Machi 23, 2026 majira ya saa moja
asubuhi.
Amesema marehemu aliyetambulika kwa jina la Mariam
Cosmas Mafumba mwenye umri wa Miaka 40, alikutwa amefariki dunia nyumbani kwake
huku uchunguzi wa awali ukionyesha kuwa alipigwa kwa kitu kigumu sehemu
mbalimbali za mwili wake ikiwemo kichwani.
“Upelelezi wa awali unaonyesha kuwa
mtuhumiwa wa tukio hilo anasadikika kuwa ni mume wake, Manyanda Mbuye, ambaye
baada ya tukio alitoroka. Jeshi la Polisi linaendelea kumtafuta ili achukuliwe
hatua za kisheria,” amesema SACP Magomi,.
Aidha, ameeleza kuwa chanzo kinachodhaniwa kusababisha
tukio hilo ni wivu wa mapenzi, ambapo mtuhumiwa alimshuku marehemu kuwa na
mahusiano ya kimapenzi na wanaume wengine.
Kamanda huyo amelilaani tukio hilo akisema ni la
kikatili na lisilokubalika katika jamii, huku akisisitiza kuwa juhudi
zinaendelea kuhakikisha mtuhumiwa anapatikana na kufikishwa mbele ya vyombo vya
sheria.
“Nitoe wito kwa wanandoa na wanaoishi
pamoja kuzingatia upendo, kuvumiliana na kutafuta suluhu ya migogoro yao kwa
njia ya amani. Kitendo cha kuua ni kosa la jinai na hakikubaliki,” amesema
SACP Magomi,.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga linaendelea na
uchunguzi wa kina kubaini ukweli wa tukio hilo huku likiwahimiza wananchi kutoa
taarifa zitakazosaidia kukamatwa kwa mtuhumiwa.
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254
Post a Comment