Na Mapuli Kitina Misalaba
Mwanafunzi mmoja wa kidato cha nne aitwaye Rebecka
Boniphace Maganga mwenye umri wa Miaka 17, anayesoma Shule ya Sekondari Old
Shinyanga, amefariki dunia kwa tuhuma za kujinyonga ndani ya chumba alichokuwa
akiishi.
Tukio hilo limetokea Aprili 27, 2026 majira ya saa
saba mchana katika eneo la Old Shinyanga, baada ya mwanafunzi huyo kudaiwa
kujinyonga kwa kutumia mkanda wa sketi ya shule.
Kamanda wa jeshi la Polisi Mkoa wa Shinyanga, Kamishna
Msaidizi Mwandamizi wa Polisi Janeth Magomi amesema jeshi la polisi lilipokea
taarifa za tukio hilo kutoka kwa mlezi wa marehemu, Mashala Piter (56),
aliyegundua kifo hicho.
Kwa mujibu wa Kamanda Magomi, uchunguzi wa awali
unaonesha kuwa tukio hilo linahusishwa na msongo wa mawazo, baada ya mwanafunzi
huyo kurudishwa nyumbani na walimu akitakiwa kurejea shuleni akiwa na mzazi
kufuatia kutohudhuria masomo kwa muda wa wiki mbili bila taarifa.
Mwenyekiti wa kitongoji cha Senyenge, Kijiji cha Old
Shinyanga, Benjamin Andrew amesema walipokea taarifa za tukio hilo majira ya
saa sita mchana na kufika eneo la tukio ambapo walimkuta mwanafunzi huyo tayari
amefariki.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Shujaa wa
Maendeleo na Ustawi wa Jamii Tanzania (SMAUJATA) Manispaa ya Shinyanga, Bi. Meryester
Nyalusanda ametoa wito kwa wazazi na walezi kujenga ukaribu na watoto wao.
Amesema ni muhimu familia kuwa na mawasiliano ya
karibu ili kubaini mapema changamoto wanazopitia watoto, badala ya kuchukua
hatua kali kabla ya kuelewa tatizo.
Mwili wa marehemu umehifadhiwa katika Hospitali ya
Manispaa ya Shinyanga kwa uchunguzi zaidi, huku jeshi la polisi likiendelea na
uchunguzi wa tukio hilo.
SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA
🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA
Wasiliana nasi:
📍 East African Spirits (T) Ltd
📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

Post a Comment