" MANKILIGO AVUTIWA NA VIPAJI VYA UNDER 20 NIACHEKONA CUP 2026, AWAHIMIZA WADAU WAJE KUJIONEA VIPAJI

MANKILIGO AVUTIWA NA VIPAJI VYA UNDER 20 NIACHEKONA CUP 2026, AWAHIMIZA WADAU WAJE KUJIONEA VIPAJI

Na Mapuli Kitina Misalaba

Ligi ya NIACHEKONA CUP 2026 inayoendelea katika uwanja wa Mwabenda uliopo kata ya Solwa, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga imeendelea kuvutia wadau mbalimbali wa michezo huku Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Shinyanga, Said Mankiligo akipongeza kiwango cha vipaji vinavyoendelea kuonekana katika mashindano hayo.

Akizungumza baada ya kushuhudia baadhi ya michezo ya ligi hiyo, Mankiligo amesema amefurahishwa na uwepo wa vijana wengi wenye vipaji vya soka hususan wa umri wa chini ya miaka 20 ambao wanaendelea kuonesha uwezo mkubwa ndani ya uwanja.

“Mimi nimefika katika kiwanja hiki kuja kushuhudia mechi za ligi ya NIACHEKONA ambayo imeandaliwa na mdau wa michezo Paul Daud maarufu MC NIACHEKONA. Ukweli nimekuja kugundua kuna vipaji vingi vya under 20 vinaonekana hapa, hii ndiyo fursa ya timu za Mkoa wa Shinyanga kuweza kujua under 20 wako wapi kuliko kwenda kugharamikia kuchukua wachezaji wenye majina makubwa ambao wakifika kwenye ligi ya mabingwa wa mikoa wanaenda kuenguliwa,” amesema Mankiligo.

Amesema viongozi wa vilabu vinavyoshiriki ligi ya Mkoa wanapaswa kutumia mashindano hayo kama sehemu ya kusaka vipaji vya vijana badala ya kutegemea wachezaji waliokwisha kupita katika kiwango cha ushindani.

“Kwahiyo nawashauri sana viongozi wa vilabu vyote vya mpira ambavyo vitashiriki kwenye ligi ya Mkoa vifike katika uwanja huu kuja kushuhudia na kujionea vipaji vilivyopo hapa. Nimekuja kugundua vijana wenye vipaji vikubwa sana, wengi wao wana miaka 17, 18, 19 hadi 20 na wakubwa ni wachache sana kwenye timu. Kwa kweli imenifurahisha sana,” ameongeza.

Aidha amempongeza mwandaaji wa mashindano hayo Bwana Paul Daud maarufu MC NIACHEKONA kwa kuendelea kutoa nafasi kwa vijana kuonesha vipaji vyao kupitia michezo huku akimtaka kuendelea kuandaa mashindano hayo hata katika miaka ijayo.

Mankiligo pia ametoa wito kwa wadau wa michezo pamoja na wananchi kujitokeza kwa wingi kushuhudia mashindano hayo ili kuendelea kuwapa hamasa vijana wanaopambana kuonesha uwezo wao wa kisoka.

Kwa upande wake Katibu wa Kamati ya Mashindano Sambayi Jilya ametangaza matokeo ya mchezo wa leo ambapo timu ya SHILIMA kutoka Mkoa wa Mwanza imeibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya SONGAMBELE MHANGU kutoka kata ya Salawe katika mchezo uliokuwa na ushindani mkubwa.

Aidha amesema michezo itaendelea kesho ambapo NYUNDO FC itashuka dimbani kuivaa NZOZA katika mchezo unaotarajiwa kuvuta mashabiki wengi wa soka ndani na nje ya Solwa.

Mashindano ya NIACHEKONA CUP 2026 yameshirikisha jumla ya timu 22 kutoka maeneo mbalimbali ikiwemo Mkoa wa Mwanza, Geita, Kahama, Manispaa ya Shinyanga pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga kwa lengo la kuibua vipaji vya vijana na kuimarisha mshikamano kupitia michezo.

Mpigie Bwana Paul Daud maarufu MC NIACHEKONA kwa huduma za ushereheshaji wa shughuli mbalimbali, matangazo na burudani unaweza kuwasiliana naye kupitia namba 0757 267 738.

Timu ya SONGAMBELE MHANGU


SHY TALENT FILMS - CONTENT YA MWISHO DRAMA

🥃🍶 TUMIA VINYWAJI BORA VYA KAMPUNI YA EAST AFRICAN SPIRITS – BEI RAFIKI, LADHA SAFI BILA HARUFU MBAYA

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254


 

Post a Comment

Previous Post Next Post