Na, Egidia Vedasto,
Misalaba Media, Arusha.
Ofisi ya Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) imetoa elimu kwa waandishi wa habari mkoani Arusha kuhusu majukumu ya ofisi na mipaka yake.
Akitoa elimu katika mafunzo hayo Mkuu wa kitengo cha habari na mawasiliano ofisi ya CAG, Focus Mauki amesema kazi ya CAG ni kukagua hesabu za serikali, kuandaa ripoti za ukaguzi na kuziwasilisha kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kabla ya kuwasilisha Bungeni kwa mujibu wa sheria.
Aidha amesema wajibu na mchango wa ofisi hiyo ni kuimarisha uwajibikaji na matumizi sahihi ya rasilimali za umma.
"Waandishi wa habari mnakumbushwa umuhimu wa kutumia taarifa za ukaguzi kwa weledi, kuhakikisha zinawasilishwa kwa usahihi bila kupotosha maudhui au kuathiri maslahi ya umma"amesema Mauki.
Katika namna hiyohiyo Mkaguzi wa nje wa hesabu za serikali Valence Lutakyamirwa ametoa rai Kwa asasi za kiraia (CSO), serikali za mitaa na halmashauri za Wilaya kuandaa nyaraka za hesabu na kutoa ushirikiano kurahisisha zoezi la ukaguzi wa hesabu vile inavyotakiwa.
Vilevile ameeleza kuwa ushirikiano kati ya CAG na vyombo vya habari una nafasi kubwa katika kuhamasisha uwajibikaji, uwazi na matumizi sahihi ya rasilimali za umma kupitia taarifa za ukaguzi.
"Wananchi Wana kiu ya kufahamu kazi zinazofanywa na ofisi ya Mkaguzi mkuu wa serikali, wanatamani kujua ni taasisi gani imekutwa na hati chafu au safi. Hatua hiyo itasaidia kuwaibua, kuwaweka wazi na kufanya taasisi zinazingatia matumizi sahihi ya rasilimali za umma"
Sambamba na hayo ameahidi kushirikiana na Waandishi wa habari bega kwa bega kuhakikisha wanaripoti taarifa ya CAG.
Kwa upande wao, Waandishi wa habari waliohudhuria mafunzo hayo, wamesema yamewaongezea uelewa kuhusu namna ya kuripoti taarifa za ukaguzi kwa usahihi na kuwasaidia kutekeleza majukumu yao kwa weledi.
Post a Comment