" USHIRIKIANO WA MISA TAN NA EWURA WALETA MATOKEO CHANYA KWA VYOMBO VYA HABARI NCHINI

USHIRIKIANO WA MISA TAN NA EWURA WALETA MATOKEO CHANYA KWA VYOMBO VYA HABARI NCHINI

 

Na Mapuli Kitina Misalaba

Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika, tawi la Tanzania (MISA Tanzania), kwa kushirikiana na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), imeendesha warsha ya tathmini ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari na wahariri, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa maazimio ya mafunzo yaliyofanyika Juni 16, 2025.

Akizungumza katika warsha hiyo leo Februari 27, 2026 jijini Dar Es Salaam, Mwenyekiti wa MISA TAN, Edwin Soko, ameishukuru EWURA kwa kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo katika kuwawezesha waandishi wa habari kuandika kwa weledi kuhusu masuala ya uthibiti wa nishati na maji.

Amesema tangu mafunzo ya awali kufanyika, jumla ya habari 103 zimeandikwa na kurushwa kupitia vyombo mbalimbali vya habari, hatua inayodhihirisha mafanikio ya ushirikiano huo.

Ameongeza kuwa MISA TAN inaishukuru EWURA kwa kuwaamini na kuahidi kuwa waandishi waliopata mafunzo wataendelea kuwa mabalozi wazuri wa taasisi hiyo popote walipo.

Katika wasilisho lake, Mwenyekiti huyo amesisitiza matarajio ya kuona habari zenye weledi, zinazozingatia maadili ya taaluma na zenye kuleta suluhisho kwa jamii huku akiwasisitiza washiriki kuendelea kuandika kwa ufasaha kuhusu majukumu ya EWURA baada ya kuifahamu vyema mamlaka hiyo, pamoja na kufanya kazi kwa karibu na ofisi za kanda za EWURA ili kupata taarifa sahihi.

Meneja wa EWURA Kanda ya Mashariki, Mhandisi Lorivii Long’idu, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA amesema jukumu la EWURA ni kuelimisha umma kuhusu masuala ya uthibiti wa huduma za nishati na maji, na kwamba kupitia vyombo vya habari wanaamini wakielimisha waandishi wa habari wanakuwa wameuelimisha umma kwa ujumla.

Ameeleza kuwa katika sekta ya nishati, kwa takwimu zilizopo nchini, huduma zinaendelea vizuri na ubora wake umeimarika ambapo amewaomba waandishi kuendelea kuwa mabalozi wazuri kwa kuandika habari za kuelimisha umma kwa kuzingatia maadili na misingi ya taaluma ya uandishi wa habari.

Aidha, amebainisha kuwa EWURA imekuwa ikitoa ushirikiano kwa waandishi wa habari na itaendelea kufanya hivyo, ili kuhakikisha wananchi wanapata elimu sahihi kuhusu haki na wajibu wao katika matumizi ya huduma za nishati na maji.

Kuhusu changamoto zilizopo, amesema baadhi ya watumiaji wa huduma hizo wamekuwa na mazoea yanayochangia malalamiko yasiyo rasmi, akiwataka waandishi kusaidia kuelimisha wananchi kuchukua hatua stahiki kwa kufikisha malalamiko yao katika ofisi za EWURA.

Ametolea mfano changamoto zinazowakabili baadhi ya wamiliki wa magari wakati wa kununua mafuta, pamoja na bili bandikizi za maji au umeme, akisisitiza kuwa malalamiko hayo yakifikishwa katika ofisi za EWURA hushughulikiwa bila gharama yoyote.

Mhandisi Long’idu amesisitiza kuwa EWURA itaendelea kushirikiana na vyombo vya habari katika juhudi za kuwafikishia wananchi elimu juu ya wajibu wao na namna bora ya kunufaika na huduma za nishati na maji.

Kwa upande wake Afisa Uhusiano na Mawasiliano kwa Umma wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Wilfred Mwakalosi, amesema bado wananchi wengi hawafahamu haki na wajibu wao katika huduma za nishati na maji, hali inayochangia baadhi yao kushindwa kudai haki zao au kutotimiza wajibu wao ipasavyo.

Amesema uelewa mdogo kwa wananchi unasababisha malalamiko mengi kutowasilishwa katika mamlaka husika kwa wakati, huku wengine wakishindwa kufuata taratibu sahihi za kupata huduma au kuwasilisha changamoto zao.

Ameongeza kuwa wananchi wakifahamu haki zao pamoja na wajibu wao, itasaidia watoa huduma kutekeleza majukumu yao kwa wakati na kwa ufanisi zaidi, sambamba na kuimarisha uwajibikaji katika sekta ya nishati na maji.

Warsha hiyo imehusisha majadiliano ya wazi, maswali na majibu kati ya washiriki na wataalamu wa EWURA, pamoja na kufikiwa kwa maazimio ya pamoja yaliyolenga kuimarisha uandishi wa habari za sekta ya nishati na maji kwa weledi na uwajibikaji. Hatua hiyo imeelezwa kuwa ni sehemu ya juhudi endelevu za kuimarisha ushirikiano kati ya MISA Tanzania na Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), kwa lengo la kuhakikisha wananchi wanapata taarifa sahihi, zenye kuelimisha na kuchochea uwajibikaji katika matumizi ya huduma za nishati na maji.

Meneja wa EWURA Kanda ya Mashariki, Mhandisi Lorivii Long’idu, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA Meneja wa EWURA Kanda ya Mashariki, Mhandisi Lorivii Long’idu, akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa EWURA 

Mwenyekiti wa MISA TAN, Edwin Soko, akiishukuru EWURA kwa kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo. 

Mwenyekiti wa MISA TAN, Edwin Soko, akiishukuru EWURA kwa kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo. 







 

  • Wasiliana nasi:
    📍 East African Spirits (T) Ltd
    📞 +255 767 650 806 | +255 652 096 254

 

Post a Comment

Previous Post Next Post