" KAMA AFYA YAKO SI NJEMA USIENDESHE GARI

KAMA AFYA YAKO SI NJEMA USIENDESHE GARI


Afya ndiyo mtaji wa kila mtu. Pale afya inapokuwa si njema, hata kazi za kawaida zinaweza kuwa hatarishi hasa kazi ya udereva wa magari ya abiria ya masafa marefu ambayo huhitaji umakini mkubwa kila wakati.

Kutokana na hilo, madereva wa mabasi ya masafa marefu wametakiwa kuhakikisha wana afya njema kabla ya kuanza safari.

Wito huo umetolewa na Sajenti David Ndimila kutoka Kikosi cha Usalama Barabarani mkoani Shinyanga, akisisitiza kuwa kuendesha gari ukiwa mgonjwa ni hatari si kwa dereva pekee, bali pia kwa abiria na watumiaji wengine wa barabara.

Ameeleza kuwa hali ya afya isiyo nzuri inaweza kusababisha matatizo kama uchovu uliopitiliza, uoni hafifu au hata usingizi, hasa pale dereva anapotumia dawa zenye madhara ya kusinzia. Hali hizi zinaweza kumfanya dereva kushindwa kulimudu gari ipasavyo na hivyo kuongeza uwezekano wa ajali.

Aidha, Sajenti Ndimila amesisitiza umuhimu wa kuwepo kwa madereva wawili katika magari ya abiria ya masafa marefu. Madereva hao wanapaswa kuwa na afya njema ili waweze kupokezana kuendesha, jambo linalosaidia kupunguza uchovu na kuongeza umakini wanapokuwa safarini.

Post a Comment

Previous Post Next Post